Tuesday, 8 December 2015

SUKARI KUTOKA NJE INAVYOUA VIWANDA VYA NCHINI


MTZ UCHUMI HII SAFI.inddMTZ UCHUMI HII SAFI.indd>>TPC wataka itozwe kodi ya asilimia 100
NA UPENDO MOSHA, MOSHI
TANZANIA ni miongoni mwa nchi zinazoendelea Afrika kupitia sekta mbalimbali za kiuchumi vikiwemo viwanda.
Licha ya umuhimu wa viwanda hivyo bado kumekuwa hakuna sera madhubuti zinazolenga kuboresha na kuendeleza
viwanda vya ndani.
Sekta hiyo bado inakabiliwa na changamoto nyingi kiasi cha kuchelewesha malengo yaliokusudiwa ya kukuza uchumi na maisha bora kwa wananchi wake.
Sera zilizopo zinaruhusu kuuzwa kwa bidhaa mbalimbali zinazozalishwa nje ya nchi na hata zile zinazozalishwa ndani lakini kumekuwa na tatizo katika bidhaa zinazozalishwa ndani.
Bidhaa ambazo zimeonekana kuteka masoko yetu nyingi zinatoka nje licha ya kwamba ziko bidhaa nyingi zinazozalishwa na viwanda vya ndani lakini zinakosa soko.
Ripoti iliyotolewa na Wizara ya Viwanda Biashara na Masoko, inaonyesha kuwa sekta ya viwanda nchini imekuwa ikikua kwa asilimia tisa tu kwa mwaka, kiwango ambacho bado ni kidogo.
Wawekezaji wa viwanda mbalimbali nchini wamekuwa wakiathiriwa katika uzalishaji kutokana na kutokuwapo kwa sera madhubuti ya kuvilinda viwanda vya ndani.
Na hii ni kutokana na baadhi ya sera hizo kuruhusu uagizwaji wa bidhaa sawa na zile zinazozalishwa hapa nchini na ambazo mara nyingi huuzwa kwa bei ya chini kuliko zinazozalishwa hapa nchini na hivyo kuathiri viwanda vya ndani.
Mojawapo ya viwanda vilivyothiriwa na hali hiyo ni Kiwanda cha kuzalisha sukari cha TPC kilichoko eneo la Langasani, wilaya ya Moshi, mkoani Kilimanjaro.
Kiwanda hiki kimekuwa kikikabiliwa na changamoto kubwa ya kushindwa kuhimili misukosuko ya soko la ndani kutokana na uagizwaji wa sukari kutoka nje ya nchi. Sukari hiyo inayoagizwa kutoka nje huuzwa kwa bei ya chini ikilinganishwa na ile inayozalishwa hapa nchini.
Ofisa Utawala wa kiwanda hicho, Jaffary Ally, anasema kiwanda hicho kilibinafsishwa na Serikali mwaka 2000 na kukabidhiwa kwa wawekezaji kutoka nchini Morishes, (Mauritius).
Anasema tangu kukabidhiwa kwa wawekezaji binafsi, kiwanda cha TPC kimepata mafanikio makubwa katika
uzalishaji lakini kimekuwa kikikumbana na changamoto ya kuathiriwa na sukari inayoagizwa kutoka nje ya nchi kiholela.
“Tumelalamika sana katika ngazi mbalimbali za uongozi hapa nchini kuhusiana na athari tunazokutana nazo
kibiashara kutokana na sukari inayoagizwa kutoka nje ya nchi na hali hii inazidi kuota mizizi,” anasema Jaffary.
Anasema sukari inayozalishwa nchini imekuwa ikishindwa kufanya vizuri katika soko la ndani kwa sababu Serikali
imeruhusu wafanyabishara kuingiza sukari kutoka nje ambayo haitozwi kodi inavyostahili.
Anasema sukari hiyo imekuwa ikiuzwa kwa bei ya chini ikilinganishwa na sukari inayozalishwa na viwanda vya hapa nchini na kwamba hali hiyo imekuwa ikididimiza uchumi wa viwanda vya hapa ndani na ule wa Taifa kwa ujumla.
“Sukari hii imekuwa ikiingizwa nchini kiholela na kodi inayotozwa ni ile ya ongezeko la thamani (VAT), hivyo
imekuwa ikiuzwa kwa bei ya chini mno tofauti na sukari inayozalishwa hapa kwetu.
Inayozalishwa kupitia viwanda vya ndani imekuwa ikiuzwa kwa bei ya juu kutokana na gharama za uzalishaji,” anasema.
Anasema wawekezaji wa ndani wanahitaji kuwa na ushindani wa soko ulio wa haki hivyo ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kuwa sukari hiyo inatozwa kodi zote zinazostahili.
Anasema viwanda vya sukari nje ya nchi huwa vinazalisha ya ziada na kupelekwa katika soko la dunia la sukari na
huko huuzwa kwa bei ya chini mno na inaponunuliwa huletwa hapa nchini na kuuzwa kwa bei ya chini na hivyo kuathiri viwanda vya ndani.
“Sukari hii wenzetu wanapoipeleka kwenye soko la dunia hairudi tena kwenye masoko yaliyomo kwenye nchi zao, baada ya kukusanya kodi, huongeza kiwango hicho cha kodi na kuwa kubwa kiasi cha asilimia 60 na 90, ili isirudishwe nchini mwao kwa vile bei itakuwa ni kubwa,” anasema.
Jaffary anasema sukari inayotoka nje ingepaswa kutozwa kodi asilimia 100 ili kulinda viwanda vya ndani.
“Cha ajabu ni kwamba kwa zaidi ya miaka 10 iliyopita sukari inayotoka nje haijawahi kutozwa kodi hata asilimia 50 ili kulinda viwanda vya ndani, achilia mbali sukari inayoingia kwa magendo,” anasema.
Ofisa huyo anasema sukari ya magendo hailipiwi VAT wala kodi ya aina yeyote hali ambayo huathiri vibaya zaidi soko la ndani na kusababisha kuathirika kwa viwanda vya ndani.
Anasema viwanda vya ndani vina uwezo wa kuzalisha sukari inayotosheleza mahitaji iwapo tu Serikali itaweka mipango madhubuti ya kuvilinda viwanda hivyo.
Anasema ni vyema Serikali ikaweka utaratibu unaofaa wa sukari hiyo kuruhusiwa kuingia nchini katika misimu
ambayo viwanda vya ndani havizalishi.
“Sukari zije wakati viwanda vyetu vya ndani havizalishi kwani tumeshuhudia meli zinazoegeshwa pembezoni mwa bahari zikiwa zimehesheni sukari kutoka katika nchi za nje na wafanyabiashara wamekuwa wakifanya hujuma ya kupaki sukari hizo kwenye mifuko ya viwanda vyetu vya ndani ili ionekane imezalishwa hapa nchini”, anasema.
Anaishauri Serikali kuongeza nguvu zaidi ya kupambana na wafanyabishara wanaoingiza sukari hiyo kwa njia isiyokuwa halali.
Anasema mahitaji ya sukari nchini kwa mwaka ni tani zaidi ya 400,000 ambapo viwanda vya hapa nchini vya TPC, Mtibwa, Kilombero na Kagera huzalisha zaidi ya tani 320,000 kwa mwaka.
Kwa mujibu wa Ofisa huyo, kati ya tani hizo kiwanda cha TPC huzalisha tani 105,000 kwa mwaka sawa na asilimia 30 ya sukari yote inayozalishwa hapa nchini kwa mwaka.
Anasema wakati wanakabidhiwa kiwanda hicho kilikuwa na uwezo wa kuzalisha tani 36,000 kwa mwaka na kwamba Serikali iliwawekea malengo kutoka kuzalisha tani hizo hadi kufikisha tani 72,000 za sukari kwa mwaka.
Hata hivyo anasema licha ya changamoto zinazowakabili wamefanikiwa kuvuka lengo hilo na sasa wanazalisha zaidi
ya tani 100,000 kwa mwaka.
“Tumejiwekea malengo ya kuzalisha tani 120,000 katika miaka mitano ijayo iwapo Serikali itaweka mazingira ya kulinda soko la ndani,” anasema.
Anasema mbali na hilo pia kiwanda hicho kimefanikiwa kuongeza kiwango cha uzalishaji wa miwa ambapo ekari moja huvunwa wastani wa miwa zaidi ya tani 140 na kwamba kuna baadhi ya mashamba hutoa zaidi ya tani 200 kwa ekari.
“Kwa sasa TPC inajivunia mafanikio makubwa na iwapo Serikali itatoa fursa ya mazingira mazuri ya ushindani
tutakuwa na uwezo wa kushindana na hata kukishinda kiwanda chochote cha uzalishaji sukari barani Afrika na hata nje ya Afrika,” anasema.Kwa upande wake Ofisa Mtendaji Mkuu wa kiwanda hicho, Robert Baizaki, anasema kwa sasa sukari imezidi kurundikana kwenye maghala kufuatia kuwapo wa sukari nyingi kutoka nje ya nchi.
“Ni vyema sasa Serikali ikadhibiti uingizwaji wa sukari kutoka nje kwa lengo la kunusuru wawekezaji na uchumi wa taifa kwa ujumla,” anasema Baizaki.
Kauli ya Serikali Mkuu wa mkoa wa Kilimanjaro, Amos Makalla, ameviagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuhakikisha wanawakamata na kuwachukulia hatua za kisheria wafanyabishara wote wanaojihusisha na uingizwaji wa sukari kiholela kutoka nje. Makala anasema uingizwaji wa sukari za magendo unaathiri kwa kiasi kikubwa
wawekezaji wa ndani wanaozalisha sukari na kwamba Serikali mkoani humo haiko tayari kulivumilia suala hilo.
Mkuu huyo pia aliahidi kushirikiana na Serikali ya Mkoa wa Tanga ili kuwakamata wafanyabishara wasio waaminifu ambao wamekuwa wakiitumia bandari ya Tanga kuingiza sukari.
“Tutaweka mikakati ya pamoja ya kuimarisha ulinzi na kuwakamata wahusika watakaobainika kufanya hivyo,” anasema.


IMETOKA MTANZANIA

Thursday, 3 December 2015

PICHA MAZISHI YA ALPHONCE MAWAZO


Mheshimiwa Edward Lowassa na Mheshimiwa Freeman Mbowe wakiwa kijijini alipozaliwa Alphonse Mawazo ambapo shughuli za mazishi zimefanyika.


Mke wa Alphonce Mawazo
Mtoto wa Alphonse Mawazo Preciuos Mawazo akionekana mwenye sura ya huzuni wakati wa mazishi ya Marehemu baba yake.
Precious Mawazo akibusu mwili wa marehemu baba yake.


Jeneza lililobeba mwili wa Alphonse Mawazo likiingizwa kwenye kaburi.


TRA YAKAMATA MAKONTENA 9 DAR



Pg 1 mbiliNA SHABANI MATUTU, DAR ES SALAAM
MAMLAKA ya Mapato Tanzania (TRA) imefanikiwa kukamata makontena tisa, mali ya Kampuni ya Heritage Limited yakiwa katika eneo la maficho ya Mbezi Tangi bovu, Dar es Salaam kinyume cha sheria.
Akizungumza kuhusu ukamataji huo akiwa eneo la tukio jana, Mkurugenzi wa Huduma na Elimu kwa Mlipa Kodi TRA, Richard Kayombo, alisema taarifa hizo walipewa na msamaria mwema.
“Taarifa za kukamata makontena hayo tulipewa na msamaria mwema aliyetuambia kwamba usafirishaji ulifanyika jana (juzi) usiku kutoka bandari kavu ya PMM iliyopo Vingunguti na kibali cha bandarini kilikuwa cha Septemba 17, mwaka huu, hivyo kilikuwa kimeisha muda wake,” alisema Kayombo.
Mkurugenzi huyo alisema kwa mujibu wa nyaraka ya bandari, inaonyesha mzigo huo ulipaswa kwenda Mamlaka ya Maeneo Maalum ya Uzalishaji Bidhaa ya Kuuza Nje (EPZ), lakini katika hali ya kushangaza ulikamatwa ukiwa Mbezi Tangi bovu kinyume na taratibu.
“Taarifa za makontena hayo zinaonyesha mwenye makontena ni Kampuni ya Heritage Limited iliyo na Tin namba 1165536501 na wakala wa forodha wa mzigo huo ni Kampuni ya Nipoc Africa Limited yenye Tin namba 105595387,” alisema Kayombo.
Alisema baada ya kupata taarifa hiyo kutoka kwa msamaria mwema, mzigo huo ulikamatwa jana na kikosi maalumu cha TRA kinachojulikana kama ‘Fast Team’ kwa kushirikiana na askari wa Jeshi la Polisi.
Kayombo alisema TRA kwa mujibu wa sheria wanatakiwa kumtafuta wakala wa mzigo huo na kama hatatokea kwa muda wa saa 24 kuanzia jana, wanaruhusiwa kufungua kontena hizo na kuangalia bidhaa zilizomo.
“Kama hatajitokeza hadi kesho (leo), tutafungua makontena na kuona bidhaa ambazo zimebebwa, kama zitakuwa halali zitataifishwa na kuuzwa, na kama zitakuwa haramu zitateketezwa kwa mujibu wa sheria,” alisema Kayombo.
Mkurugenzi huyo alisema kwamba katika hatua ya awali wamebaini mmiliki wa eneo hilo la Mbezi Tangi bovu ambalo si rasmi, ndiye mmiliki wa bandari kavu ya PMM iliyopo Vingunguti.
IMETOKA MTANZANIA

MAUAJI YA KINYAMA GEITA

NA VICTOR BARIETY, GEITA
MAUAJI ya kinyama ambayo yanahusishwa na imani za kishirikina yameanza kurejea mkoani Geita, baada ya watu wanne wa familia moja wakazi wa kijiji cha Bugalama wilayani Geita kuuawa.
Watu ambao majina yao hajatambuliwa mara moja, wameuawa kwa kuchinjwa shingo kama kuku.
Waliouawa katika tukio hilo lililotokea Desemba Mosi, ni wanawake watatu na mtoto mmoja.
Kamanda wa Polisi Mkoa wa Geita,Latson Mponjoli alipoulizwa jana alikiri  kutokea kwa tukio hilo.
Akisimulia tukio hilo, Kamanda Mponjoli alisema hivi karibuni mkazi wa kijiji hicho, Samweli Masibo alifariki dunia,baada ya kuugua maradhi ya kawaida.
Alisema marehemu Masibo alikuwa na wake watatu na siku chache baada ya kufariki dunia alianza kuonekana kwa njia za kishirikina nyumbani kwa mke wa pili ambaye kwa sasa ni marehemu.
“Wanasema eti marehemu alikuwa anaonekana usiku nyumbani kwa mke wa pili na kwamba hakufariki,  bali aliuawa kishirikina masuala ambayo sisi hatuwezi kuyathibitisha’’alisema Kamanda Mponjoli.
Alisema  jana (juzi) wakati familia hiyo ikiwa inaota moto  usiku lilitokea kundi la watu ambao hawakujulikana mara moja, wakiwa na silaha za jadi na kuanza kushambulia kila mtu aliyekuwa mbele yao na kusababisha vifo  hivyo.
‘’Kwa kweli hili tukio linasikitisha,wameuawa kinyama wametenganishwa vichwa na kiwiliwili…polisi tumeanza kuchukua hatua.Tunaomba mtuvumilie kesho (leo) tutawapa majina yote ya marehemu,’’alisema mponjoli.

INATOKA MTANZANIA

JINSI MABILIONI YALIVYOCHOTWA


MTZ Alhamisi new july.inddFredy Azzah, Dar es Salaam
WAKATI Watanzania wakiumiza kichwa kujua watu waliofaidika na rushwa ya Sh bilioni 12 (dola za Marekani milioni 6), zilitokana na mkopo wa dola za Marekani milioni 600 (Sh trilioni 1.3), ambao Tanzania iliomba kwenye Benki ya Standard kupitia mshirika wake Stanbic Tanzania, imebainika kuwa mchakato ulianza mwaka 2011 na kushirikisha watu mbalimbali wakiwamo maofisa wa Serikali na watoto wao.

KESI ILIVYOANZA
Mwenendo wa kesi iliyotolewa hukumu Novemba 30 nchini Uingereza, unasema tangu mwaka 2011 Serikali ya Tanzania ilifanya juhudi za kupata mkopo wa miradi ya miundombinu kupitia soko la kimataifa la hati fungani bila mafanikio kutokana na kile kilichoelezwa ni kukosa vigezo.
Mwenendo huo unasema, benki ya Standard na Stanbic kwa pamoja zikachukua jukumu la kutafuta mkopo huo kwa Serikali ya Tanzania kupitia waziri wa fedha wa wakati huo ambaye alikuwa Mustafa Mkulo.
“Pendekezo lilikuwa Standard na Stanbic iwasilishe wazo la kuiwezesha Serikali kupata mkopo, na lilikuwa liwasilishwe kwa waziri wa fedha kwa sharti kwamba Standard na Stanbic kwa pamoja zipokee ada ya asilimia 1.4 kwa kuandaa na kuwezesha mkopo huo.
“Standard na Stanbic zilisema kwamba wazo lao hilo litauzwa kama mchakato binafsi kwa mujibu wa sheria na mwongozo wa usalama wa Marekani,” unaeleza mwenendo huo wa kesi.
Katika barua pepe ya Februari 25, 2012, Kaimu Mkuu wa Masuala ya Uwekezaji wa Stanbic, Shose Sinare, aliwafahamisha watu fulani ndani ya Standard na Stanbic, akiwamo Mkuu wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji wa Standard na Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic, kwamba wazo lao limekubaliwa na waziri wa fedha.
Kwa herufu kubwa na maandishi manene, Sinare ambaye kwenye mwenendo wote huo ametajwa kwa nafasi yake bila kugusia jina lake, alibainisha kwamba watapata asilimia 1.4 kama ada ya kuwezesha mpango huu kwa Serikali ya Tanzania.
Mwenendo huo unasema kuwa Mei 2012, kabla ya wazo la mpango huo kusainiwa, Waziri wa Fedha, Mkulo aliondoshwa na nafasi yake kuchukuliwa na waziri mwingine (Dk. William Mgimwa).
“Kuanzia Mei 2012 kuelekea mwishoni mwa mwaka 2012, Standard na Stanbic zilijaribu kufufua mpango huo kupitia juhudi zilizofanywa na Sinare na Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic (Bashir Awale), ambao walikutana na maofisa wa Serikali nchini Tanzania.
Mkuu wa Kimataifa wa Madeni ya Mitaji ya Masoko alikuwa akifahamishwa hatua kwa hatua ya maendeleo hayo na Standard, pamoja na timu ya ndani ya ushauri iliyohusika kuandaa nyaraka za mpango huo.
Juni 2012, Sinare aliwasilisha kwa ofisi ya Waziri wa Fedha  nakala ya mpango huo, ukiendelea kuonyesha Standard na Stanbic kwa pamoja kama maneneja viongozi wa mpango huo, wakitarajia kupokea ada ya asilimia 1.4 ya sehemu ya mkopo huo.

MTOTO WA WAZIRI ALIVYOAJIRIWA
Julai 2012, Stanbic ilimuajiri mtoto wa kiume wa waziri huyo mpya wa fedha.
Agosti 29, 2012, Sinare alimwandikia barua pepe Mkuu wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji wa Standard, kwamba yeye na Bashir wamefikia ‘mahali pazuri’ baada ya mkutano mzuri na Waziri wa Fedha na timu yake, na kwamba kwa sasa wako katika mwelekeo mzuri wa kusaini makubaliano ya mpango huo.
Mwenendo wa kesi hiyo unasema Sinare pia alimfahamisha Mkuu wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji wa Standard, kwamba mkutano na Waziri wa Fedha ulithibitishwa utafanyika Septemba 18.
“Septemba 4, Kaimu Mkuu wa Uwekezaji wa Benki ya Stanbic (Sinare) alimtumia Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic (Bashir) na mtoto wa kiume wa Waziri wa Fedha pendekezo la mpango wa kutafuta mkopo, na kumtaka mtoto wa Waziri wa Fedha kuziwasilisha nyaraka kwa Ofisi wa Waziri wa Fedha, kitu alichofanya siku iliyofuata.

EGMA ILIVYOINGIA
“Suala hili jipya kwa mujibu ya barua ya pendekezo la mpango huo lilikuja na ada mpya ya asilimia 2.4 ya mkopo wa dola milioni 600 Tanzania ilizoomba. Nyaraka hizo pamoja na mambo mengine zilieleza Meneja Kiongozi ni Stanbic na Standard, kwa kushirikiana na mshirika wa ndani.
“Kwamba Stanbic imlipe mshirika wa ndani, ambaye Standard ilibaini baadaye kuwa alikuwa EGMA, ada ya asilimia moja ya mkopo, kutoka jumla ya ada ambayo iliongezwa kutoka asilimia 1.4 hadi asilimia 2.4,” unaeleza mwenendo wa kesi hiyo.
Mwenendo huo unasema katika barua ya Septemba 20, 2012, kutoka kwa Mkuu wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji wa Standard kwenda kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic na Kaimu Mkuu wa Uwekezaji wa Stanbic, alieleza kwamba wanafanyia kazi barua ya upande wa pili baina yao na washirika wao, kuonyesha namna ada itakavyogawanywa na wajibu wa kila mmoja katika suala hili.
Mwenendo huo unasema kuwa wakati timu ya mkakati ya Standard ilipomjibu Sinare kwamba mshirika wa ndani (Kampuni ya EGMA) anahitaji kusaini barua ya dhamana, Sinare alijibu huku nakala ikienda kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic na Mkuu wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji, kwamba: “Hapana. Lengo ni kuwaleta kupitia makubaliano ya pembezoni baina yetu na mshirika.
“Katika michakato mingine iliyofanyika (Serikali na benki nyingine) na kadhalika. Hii ndiyo namna inavyofanywa. Serikali inapenda kuhusiana na upande mmoja tu, ambao baadaye kwa njia zake huingiza na kuendesha au kuratibu mshirika au washirika wengine.”

UZEMBE ULIOFANYIKA
Kwa mujibu wa mwenendo huo wa kesi, benki ya Standard ilionyesha uzembe kwa kutochukua hatua yoyote kufahamu uhusika wa EGMA katika mchakato wa uwezeshaji mkopo, ambao ulishuhudia ikilipwa ada ya dola milioni sita na hakuna kumbukumnbu za mawasiliano miongoni mwa maofisa wa Standard na Stanbic kuhusu umiliki wa EGMA, ushirikiano wake kwa Serikali ya Tanzania au kwanini ilifanywa kuwa sehemu ya mchakato huu.
“Septemba 20, 2012, Kaimu Mku wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji, Mkurugenzi Mtendaji wa Stanbic na Kaimu Mkuu wa Masuala ya wa Uwekezaji wa  Stanbic walifanya mkutano kwa njia ya simu kujadili  mgawanyo wa ada na EGMA.
“Katika mkutano huo pamoja na mambo mengine liliibuka suala kwamba Standard haingeweza kuilipa EGMA bila kupitia mchakato wa ‘Mjue Mteja Wako’ (KYC) kutathimini utambulisho wa mteja huyo.
“Mwishowe ikakubaliwa baina ya maofisa hao watatu kwamba ni Stanbic pekee itakayoendesha mchakato wa KYC kuhusu EGMA.
“Katika mkutano huo wa simu, Mkuu wa Masuala ya Kimataifa wa Madeni ya Masoko ya Mitaji pia alieleza kwamba; ‘nadhani hakuna haja ya kuendesha mchakato wa KYC kwa jamaa hawa na ninadhani mmefanya kazi nao na hivyo mnawafahamu vilivyo jamaa hawa’.
“Katika mkutano huo wa njia ya simu pia ulikubaliana ada nzima kuwa asilimia 2.4 ya mkopo wa dola milioni 600.

SEKESEKE LA MGAWO
“Kwamba Stanbic itailipa EGMA mgawo wake wa asilimia moja na kugawa mgawo mwingine uliobakia wa ada ya 1.4 kwa Standard.
“Kutokana na makubaliano hayo, Standard haikuwa mtia saini wa makubaliano ya ada hiyo na EGMA. Katika mawasililiano mengine ya simu Septemba 26, 2012, washiriki hao hao watatu walikubaliana kwamba kwa vile EGMA haitahusika kwa vyovyote kama Meneja Kiongozi, inahitaji kutotajwa kabisa katika barua ya dhamana ya kuendesha mpango huo na Serikali,” unaeleza mwenendo huo.
Unaongeza: “Kwa ombi la Stanbic, Standard ilishiriki kikamilifu katika kuandaa makubaliano ya ushirikiano baina ya Stanbic na EGMA. Kati ya Septemba 2012 na Februari 2013, Stanbic na Standard zilirekebisha vipengele kadhaa katika makubaliano ya ushirikiano. Mkataba huo wa ushirikiano ulieleza majukumu ya EGMA kuhusu mchakato huo wa mkopo. Lakini hakuna ushahdi wowote kuonyesha EGMA ilifanya majukumu hayo.

SERIKALI ILIVYOBARIKI DILI
“Serikali kupitia Waziri wa Fedha, ilipitisha barua ya dhamana, inayotoa dhamana au mamlaka kwa Standard na Stanbic kuwezesha upatikanaji wa mkopo kwa ajili yake Novemba 15, 2012.
“Ikaziteua Standard na Stanbic kuwa Meneja Kiongozi kuhusiana na mkopo huo. Barua ya dhamana ilihusisha ‘ada ya uwezeshaji’ ya asilimia 2.4, lakini haikueleza popote mshirika yeyote wa ndani wala upande wa tatu. Barua ya ada ya Meneja Kiongozi ilionyesha kwamba ada ya asilimia 2.4 italipwa kwa Standard na Stanbic wakiwa kwa pamoja kama mameneja kiongozi kwa ushirikiano na mshirika wake. “Ijapokuwa, barua ya ada iligusia ‘mshirika wa ndani’,  EGMA haikubainishwa kama mshirika wa ndani.”.

MAWASILIANO TATA
Mwenendo huo unasema Februari 25, 2013, Mkuu wa Masuala ya Kimataifa ya Madeni ya Masoko ya Mitaji alishiriki katika mawasiliano ya njia ya simu na wenye kuonyesha mwelekeo wa kuwekeza nchini Tanzania kupitia hati fungani.
“Wawakilishi wa Serikali ya Tanzania ambao walikuwa katika mawasiliano hayo walihusisha Waziri wa Fedha, pamoja na Kamishina wa TRA, ambaye alikuwa mwanahisa wa EGMA.
“Katika mawasiliano hayo ya simu, Mkuu wa Masuala ya Kimataifa wa Madeni ya Masoko ya Mitaji alieleza kwa muhtasari suala hilo bila kugusia kabisa EGMA, wala uhusiano wa wanahisa wake kwa Serikali, wala kuonyesha majukumu yake katika suala hilo na iwapo itapokea ada ya dola milioni sita.
“Standard haikubainisha uhusika wowote wa EGMA na ada ambayo itapokea. Standard ilisaidia kuandaa mpango wa ada ambao Serikali ilikubali kuilipa Standard, Stanbic na mshirika (EGMA) ya asilimia 2.4, bila kugusia au kufafanua kuhusu EGMA,” unasema mwenendo huo.

DILI LILIVYOKAMILIKA
Unasema Februari 27, 2013, Serikali ya Tanzania ilitoa hati zake fungani zisizoorodheshwa kupitia sheria ya uwekezaji binafsi na kupata mkopo wa dola milioni 600, zilizoingizwa katika akaunti yake mjini New York Machi 8, kisha ilihamisha ada ya asilimia 2.4 sawa na dola za Marekani milioni 14.4 kwa Stanbic Tanzania.
“Stanbic ikaipatia EGMA asilimia moja katika akaunti ya EGMA iliyofunguliwa Stanbic. Baada ya EGMA kufanya malipo ya gharama za kisheria zinazohusiana na fedha hizo, karibu dola milioni 5.2 za zile milioni sita zikachotwa kati ya Machi 18 na 27, 2013. Standard haikufahamu uwapo wa fedha hizo hadi pale zilipochotwa na haina ufahamu wowote wa malengo ya waliozichota,” unasema mwenendo huo.

KAULI YA IKULU
Juzi, katibu Mkuu Kiongozi, Balozi Ombeni Sefue, aliwaeleza waandishi wa habari kuwa Septemba 29, 2015, Mkuu wa Idara ya Uchunguzi wa Makosa Makubwa ya Ufisadi ya Uingereza (SFO), aliiandikia Benki Kuu ya Tanzania (BoT), akiomba ushirikiano kwenye uchunguzi na uendeshaji wa kesi dhidi ya Standard Bank Plc, ambayo sasa inajulikana kama ICBC Standard Bank Plc.
Alisema Oktoba 29, 2015, Benki Kuu, iliiandikia SFO kutoa taarifa kuhusu ukaguzi lengwa ambao BoT iliufanya tarehe 15 – 19 Julai, 2013 kwenye Benki ya Stanbic Tanzania.
“Ushahidi huo kutoka Benki Kuu ulikuwa sehemu ya ushahidi uliosaidia SFO kushinda kesi. Katika kipindi chote ambacho SFO ilikuwa inafanya uchunguzi, ilishirikiana na taasisi zetu ikiwamo Takukuru, Benki Kuu, FIU na wengine. Mafanikio haya ndiyo yaliyosababisha uamuzi wa Tanzania kurejeshewa dola milioni 7 (Sh bilioni 15),” alisema Sefue.
Alisema baada ya ushindi huo, uchunguzi unaendelea ndani ya nchi ili kujua dola milioni sita zimekwenda wapi, na kama zilitumika kumhonga mtu ajulikane aliyeongwa.
“Katika hili tutaomba ushirikiano wa wenye kampuni hiyo ya EGMA ambao kwa taarifa za vyombo vya habari vya Uingereza ni Harry Kitilya aliyekuwa Kamishna Mkuu wa Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA), Fraten Mboya  ambaye ni marehemu na Gasper Njuu,” alisema Sefue.
 IMETOKA MTANZANIA

Rais Magufuli atoa wiki kwa wafanyabiashara kulipa kodi

Rais John Magufuli akizungumza na wafanyabiashara Ikulu
Rais John Magufuli akizungumza na wafanyabiashara Ikulu

RAIS John Magufuli ametoa siku saba kwa wafanyabiashara walioingiza mizigo yao bila kulipa kodi wakalipe kwani baada ya hapo watachukuliwa hatua kali za kisheria. Anaandika Erasto Masalu … (endelea).
Hayo yamesemwa leo Ikulu, jijini Dar es Salaam na Rais Magufuli alipokutana na wadau wa sekta binafsi. Siku hizo sana zinaanzia leo Desemba 3, 2015.
Mkutano huo wa Rais Magufuli na wafanyabiashara hao ni sehemu ya kutumika ahadi yake ya kukuza uchumi kupitia kwa kupitia sekta binafsi, aliyoiahidi wakati wa kampeni zake.
Rais Magufuli amesema katika kipindi cha miaka mitano ya utawala wake amedhamiria kuijenga nchi na watu wasimuelewe vibaya kwa maamuzi anayofanya kwani ni kwania njema ya kuleta maendeleo na siyo ujeuri.
Pamoja na hayo Rais Magufuli amewaahidi wadau wasekta binafsi ushirikiano mkubwa kwani anatambua mchango wao katika kukuza uchumi na pia amewataka wadau hao kuwa wazalendo na kuliacha kukwepa kulipa kodi ili tuweze kujenga taifa lenye maendeleo makubwa ya kiuchumi.
Rais Magufuli amewahakikishia wafanyabiashara hao kuwa watakapokuwa tayari kuwekeza wafanye hivyo kama akikwamishwa na mtu aliyechini ya uteuzi wake basi mtu huyo ataondoka, kwani sasa ni wakati wa wadau wa sekta binafsi kuanza kuanzisha viwanda mbalimbali vitakavyotoa ajira.
Pia Rais Magufuli amewapa mawazo ya kibiashara wadau wa sekta binafsi kuanzisha kampuni ya kutenganisha udongo unaotoka kwenye machimbo ya madini, kuanzisha viwanda vya samaki pembezoni mwa bahari pamoja na kutengeneza samani zitokanazo na mazao ya misitu.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Taasisi ya Sekta Binafsi (TPSF), Regnald Mengi amesema kuwa wako tayari kumpa ushirikiano mkubwa rais katika kuhakikisha uchumi wa Tanzania unakuwa kwa haraka.
Mengi pia amemuomba rais kuendelea kukemea masuala ya rushwa pamoja kusaidia kupunguza utitiri wa kodi.

IMETOKA MWANAHALISI

PROF.LIPUMBA AKUTANA NA MAGUFULI

Rais John Magufuli akizungumza na Aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba Ikulu jijini Dar es Salaam
Rais John Magufuli akizungumza na Aliyekuwa Mwenyekiti wa CUF, Prof. Ibrahim Lipumba Ikulu jijini Dar es Salaam

Safari ya Prof. Lipumba kuwa waziri yaiva

PROF. Ibrahim Lipumba, aliyekuwa mwenyekiti wa Chama cha Wananchi (CUF), ameachiwa huru na mahakama ya Hakim Mkazi, jijini Dar es Salaam. Anaandika Yusuph Katimba … (endelea).
Mkurugenzi wa Mashitaka ya Jinai nchini (DPP), imewasilisha hati maalum mahakamani hapo kueleza kutokuwa na dhamira ya kuendelea na mashitaka yanayomuhusu Prof. Lipumba na wenzake.
Prof. Lipumba ameachiwa huru siku tatu baada ya kukutana na John Pombe Magufuli, Ikulu jijini Dar es Salaam. Prof. Lipumba alikutana na Magufuli, Ikulu jijini Dar es Salaam, tarehe 30 Novemba.
Mara baada ya kuwasilisha hati hiyo mahamani, Cyprian Mkeha, hakimu aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo, ameamuru kufutwa kwa kesi hiyo na kuamuru kumwachia huru.
Prof. Lipumba alikuwa akitetewa mahakamani na Peter Kibatala. Wakili huyo alieleza mahakama kutokuwa na pingamizi na hatua hiyo.
Prof. Lipumba na wafuasi 30 wa chama hicho walishitakiwa kwa madai ya mkusanyiko usio halali, tarehe 22 na 27 Januari mwaka huu, wilayani Temeke.
Mkusanyiko huo ulikuwa maalum kwa ajili ya kumbukumbu ya mauaji wa 15 waliouawa Unguja na Pemba, Januari 26 na 27 mwaka 2001.
Mongoni mwa wafuasi hao, ni pamoja na Shabani Ngurangwa (56), Shabani Tano au Kasakwa (29), Shabani Polomo (40), Juma Mattar (54), Mohammed Kirungi (40), Athumani Ngumwai (40), Shaweji Mohamed Mketo (39) na Abdul Juma Kambaya (40).
IMETOKA MWANAHALISI FORUM